Sunday, December 28, 2008

MATUKIO YA NYUMA KALOLENI

Chemichemi ya Goa inayohudumia wakulima lukuki inavyooneka mwezi wa Novemba. Panahitajika usafi hapa

Watoto wanaogolea kujiburudisha eneo la chemichemi ya Goa
Kuna uchafu umejikusanya ndani ya chemichemi ya Goa. Patasafishwa hivi karibuni


Diwani wa Kata ya kaloleni mwenye t-shirt nyeupe akizungumza na wakulima wa mpunga wa Kaloleni juu ya maendeleo yao.




Wakulima wa Kaloleni wakimsikiliza diwani wao alipofanya nao mkutano wa hadhara kubadilishana mawazo mwezi wa October.




Wednesday, December 24, 2008

UJENZI WA ZAHANATI UNAVYOENDELEA


Fundi akiwajibika

Mratibu wa TASAF Moshi Manispaa akiwa eneo la ujenzi kuratibu kazi pamoja na mhandisi na mwenyekiti wa Kamati ya Ujenzi mwenye shati la light bluu.

Mafundi mzigoni

Mhandisi wa Tasaf akielekeza mafundi pamoja na wanakamati ya ujenzi ukorogaji mzuri wa zege

Mhandisi akimgombeza mmoja wa mafundi kwa kutozingatia maelekezo

MAMBO YALIVYOKUWA MARIALE CUP


Wageni wakiongozwa na Aggrey Mariale wakienda jukwaani baada ya ukaguzi wa timu.

Bibie wachezaji wa Kilimanjaro Queens wakifurahia ushindi wa Netiboli

Kapteni wa Kaloleni United akikabidhiwa kikombe

Tuesday, December 9, 2008

KALOLENI YASHINDA FAINALI TAMASHA LA MANGI MARIALE

Kilimanjaro Qeens wakipata Kikombe na Mbuzi
Siku ya Ufunguzi wa michezo hiyo wanakaloleni, akina dada wa netiboli
Kikombe kwa kapteni wa Kaloleni United
Mabingwa wa mwaka huu Kaloleni United.
Timu ya Soka ya Kata ya Kaloleni, Kaloleni United imeshinda tamasha la mwaka huu la Mangi Mariale na kukabidhiwa Kikombe, jezi, mipira minne pamoja na ng'ombe dume baada ya kuishinda timu ya Langasani kwa bao moja kwa bila katika Uwanja wa Chuo cha Ushirika Moshi.
Pia timu ya Kilimanjaro Queens ilishinda upande wa netiball kwa kupata Kikombe na Mbuzi.

Wednesday, December 3, 2008

UJENZI WA ZAHANATI UNAENDELEA VIZURI SANA

Hapa jengo la zahanati ya Kata kupitia TASAF linapandishwa kuta zake.
Baada ya hatua ya msingi ujenzi wa kujenga kuta ulianza, hapa mafundi na wananchi waliojitokeza wakifanya kazi


Ujenzi unaanzia hatua ya msingi.

Msingi unaimarishwa kwa kujazwa mawe kama inavyoonekana.



Katika Kata ya Kaloleni ni miradi kwa kwenda mbele. Mradi wa ujenzi wa zahanati ndio umeshika kasi hasa. Pichani juu ni baadhi ya hatua za mradi kuanzia hatua ya msingi hadi hivi saa. Inategemewa mapema mwakani watu wataannza kutibiwa hapa.








Sunday, November 30, 2008

UJENZI WA MFEREJI WAANZA


Kupitia mpango wa maendeleo ya kilimo ya wilaya (DADP) Halmashauri ya Manispaa ya Moshi inajenga mfereji wa umwagiliaji katika eneo la Goa kwa ajili ya wakulima wa Mpunga wa Kaloleni.

Tuesday, November 25, 2008

MIRADI INAYOFANYIKA KATA YA KALOLENI KWA SASA







Kuna miradi kadhaa inayoendelezwa katika Kata ya Kaloleni kwa sasa. Panajengwa mfereji wenye urefu wa meta 1470 katika Kitivo cha kilimo cha mpunga eneo la chemichemi ya Goa.

Friday, November 21, 2008

Kwenye kata ya Kaloleni kwa sasa kuna mambo mengi tu ya kimaendeleo ambayo yanaendelea. Kwa mfano, kuna ujenzi wa miradi kama elimu, kilimo na afya.

Kuna ujenzi wa mfereji wa umwagiliaji, ujenzi wa madarasa shule ya sekondari Msasani, Ujenzi wa uzio wa shule ya Msingi Kaloleni na ujenzi wa Zahanati ya Kata.

Unaweza ukajionea mapicha kuthibitisha haya:

Friday, August 15, 2008

IFAHAMU KATA YA KALOLENI

PICHANI JUU: MKUU WA WILAYA YA MOSHI- HALMASHAURI YA MANISPAA, NDUGU: MUSA SAMIZI AKIKABIDHI HUNDI YA SHILINGI MILIONI THELATHINI NA SABA KWA MWENYEKITI WA MTAA WA KALIMANI MZEE MOULID KIMEY NA DIWANI WA KATA YA KALOLENI NDUGU MICHAEL MWITA KWA AJILI YA UJENZI WA ZAHANATI YA KATA YA KALOLENI INAYOJENGWA KWA UTARATIBU WA M FUKO WA MAENDELEO YA JAMII (TASAF).
UJENZI UNATARAJIWA KUKAMILIKA MWISHONI MWA MWAKA HUU (2008).
ENEO:

Kata ya Kaloleni inapatikana pembezoni mwa Halmashauri ya Manispaa ya Moshi katika Mkoa wa Kilimanjaro. Ipo kilometa nne (4) kusini mashariki mwa mji wa Moshi. Kaskazini imepakana na Kata ya Njoro, kusini imepakana na Kata ya Mabogini na Mashariki imepakana na Msitu wa Rau na upande wa Magharibi imepakana na Kata ya Pasua.

Kupitia mitaa yake miwili: KALIMANI na KALOLENI, Kata inajumuisha maeneo ya makazi ambayo yamepimwa kisheria pamoja na maeneo mengine ambayo wakazi wanaishi pasipopimwa yaani Kalimani na baadhi ya eneo la Kaloleni. Kata pia imezungukwa na dampo la taka zote za Manispaa upande wa ……….

IDADI YA WATU

Kata ya Kaloleni ina mitaa miwili ambayo ni Kaloleni na Kalimani. Kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2002, Kata ya Kaloleni ina wakazi 5520: wanawake ni 2709 na wanaume ni 1509. Wakazi wake ni mchanganyiko wa makabila hasa Wapare, Wachaga na Wasambaa.

SERIKALI YA KATA

Kata ya Kaloleni iko chini ya Afisa Mtendaji wa Kata ambaye ni mwakilishi wa Mkurugenzi wa Manispaa ya Moshi. Afisa Mtendaji wa Kata anaratibu shughuli zote za maendeleo ya Kata chini ya Kamati ya Maendeleo ya Kata (WDC) ambayo iko chini ya Uenyekiti wa Diwani wa Kata.
Kamati ya Maendeleo inawajumuisha Wenyeviti wa Mitaa pamoja na Maafisa watendaji wa Kata pamoja na maafisa wengine wote ndani ya Kata kama: Mratibu wa Elimu, Afisa Afya wa Kata, Afisa Maendeleo, pamoja na Afisa Kilimo wa Kata.


ARDHI

Ardhi ya Kaloleni imegawanyika katika maeneo ya kuishi yaliyopimwa katika kitongoji cha Msasani, shughuli za kilimo cha mpunga zenye ukubwa wa hekta 118 pamoja na maeneo matatu ya wazi yaliyotengwa.

Kazi mbalimbali zinafanywa chini ya uratibu wa Kamati ya Maendeleo ya Kata ya Kaloleni. Pamoja na udogo wa Kata hii, kuna mambo mengi sana na ya msingi yanayofanyika ndani ya Kata hii:

a) KILIMO CHA MPUNGA
Yanapatikana mashamba ya mpunga ndani ya Kata. Hapa wakulima wanatoka ndani ya Kata na wengine wanatoka Kata za jirani hasa Pasua na Njoro. Kilimo hiki kinasaidia sana wakulima kuweza kujikwamua na umasikini. Kilimo cha Mpunga kinaendeshwa kwenye vitivo vikuu viwili: Njoro ya Goa na Njoro ya Liwali.
Sekta ya umwagiliaji imeendelea kuboreshwa kwani serikali kupitia mpango wa maendeleo ya Kilimo ya Wilaya (DADP) imeidhinisha kiasi cha shilingi 23,816027 katika ujenzi na ukarabati wa mifereji ya umwagiliaji maji ili kuboresha kilimo cha mpunga katika Kata.

SHUGHULI NDOGONDOGO

Pamoja na mpunga, mazao mengine hulimwa katika Kata ya Kaloleni ingawa si kwa kiwango kikubwa. Mazao hayo ni mahindi, maharage, mboga za majani, miwa na magimbi. Pia kuna ufugaji wa ng’ombe, mbuzi, kondoo, nguruwe na kuku ambazo hufanyika majumbani kwasababu ya ukosefu wa maeneo ya kulishia.

b) USTAWI WA JAMII

1.
Biashara na Masoko

Kikao cha Baraza la Madiwani katika kikao chake cha tarehe 22.12.07 kiliidhinisha soko la Kaloleni kuwa soko la jumla. Tayari vibanda 92 vimepimwa na ramani ziko tayari; ofisi ya Mtendaji inaendelea na ufuatiliaji wa hatua za mwisho ili wahusika wapewe taratibu za ujenzi.

2. Ushirika na uwezeshaji

Kata ya Kaloleni inao ushirika wa kuweka na kukopa (SACCOS) iliyosajiliwa kwa usajili no. …….Ina wanachama …………. Na mtaji wa Tshs………….. chini ya uenyekiti wa Ndugu Paul Felix Rambau. Hadi sasa kuna wanachama mia moja na lengo ni kuwa na wanachama 3000.
Inatarajiwa kukopa shs. Milioni 40 katika Benki ya CRDB na fedha hizo zitakopeshwa wanachama.

3. Mikopo kwa Wajasiriamali

Wananchi wa Kaloleni wanajipatia mikopo kupitia Benki ya Akiba pamoja na benki zingine kwa ajili ya kujiwezesha kibiashara katika nyanja tofauti.

4. Miradi ya Uwezeshaji

Kata ya Kaloleni kupitia Mfuko wa Uwezeshaji (TASAF) inatarajia katika kipindi cha mwaka 2008 – 2009 kuendesha miradi chini ya Tume ya Kudhibiti Ukimwi (TACAIDS) ili kuwawezesha miongoni mwa wakazi mbalimbali kimaisha. Miradi hiyo itagusa wakazi wa mazingira magumu, Walemavu, Wajane na Wagane, Waathirika wa Ukimwi, Mayatima, pamoja vikundi vya vijana vinavyoelimisha rika na watoa huduma kwa waathirika majumbani.

c)
AFYA

Halmashauri ya Manispaa tayari imeidhinisha Tsh. 39, 955,600/= kupitia mradi wa TASAF ili ujenzi wa Zahanati uanze. Akaunti imeshafunguliwa na tayari Mkuu wa Wilaya alizindua rasmi mradi wa ujenzi tarehe 05/08/2008. Inatarajiwa hadi mwisho wa mwaka huu mradi utakuwa umekamilika.




Pamoja na ukosefu wa zahanati, wananchi wa Kaloleni wanapata huduma za afya kupitia Taasisi ya Muslim Agency ambayo ipo ndani ya Kata. Na pia kupitia zahanati ya jirani kwenye Kata ya Pasua.

d)
UKIMWI

Kupitia ushirikiano na asasi zisizo za kiserikali tayari wananchi wanapima afya zao.

-Pia Shirika la KIWAKKUKI limefadhili familia ishirini na nne (24); 12 kila mtaa. Hizi ni familia zilizotambulika kuwa zinalea ama kuishi na watoto yatima wenye umri chini ya miaka nane. Ufadhili huo ni mkopo bila riba wa shs. 100,000 kwa kila familia. Tayari familia 21 zimepokea fedha hizo na kujiunga na Saccos ya Kata ili kukuza mitaji yao.

Familia nyingine tayari zinaendelea kutambuliwa na pindi marejesho yanapotosheleza kufikia shilingi laki moja kila mwezi basi familia mpya huongezwa katika mradi huo wa kuwawezesha walezi hao. Hadi mwanzoni mwa mwezi August tayari familia nyingine tatu zimeongezwa katika mradi huo wa KIWAKKUKI na sasa kuna familia ishirini na saba (27).
-Pia katika shule ya Sekondari kuna wanafunzi yatima 54: miongoni mwao, 12 kati yao wanafadhiliwa na wahisani mbalimbali.

e)
MAJI

Kuna vyanzo kadhaa vya maji katika Kata ya Kaloleni. Hivi ni Chemichemi ya Goa, Liwali,………….. hizi zote hutegemewa kwa ajili ya maji ya kilimo cha mpunga na mbogamboga na pia maji ya matumizi ya nyumbani katika chemichemi ya Goa.
Kupitia mpango wa National Rural Water Supply & Sanitation Programme, Kata ya Kaloleni ilipewa Tsh. 21,000,000 kupitia manispaa na Muwasa ili kusambaza maji safi na ujenzi wa vilula vya maji. Kazi hiyo imekamilika kwa vilula viwili kujengwa eneo la Kalimani kwa Kidelio na Kaloleni kwa Aidano.
-Mabomba ya maji yamepitishwa karibu na Makazi ya watu kuwawezesha kupata huduma ya kuvuta maji kwa urahisi. Lengo ni kuwezesha zaidi ya watu 800 kupata maji safi na salama.

f)
BARABARA

Barabara rasmi za kudumu ni tatizo katika Kata ya Kaloleni; tayari mpango wa ukarabati wa barabara za Kata umewasilishwa Manispaa na kamati ya Maendeleo ya Kata kwa ajili ya utekelezaji katika bajeti ya 2008 – 2009. Mipango ya hiyo ya maendeleo licha ya barabara inajumuisha pia:
i) Ujenzi wa mifereji ya maji ya mvua – Kaloleni
ii) Ujenzi wa Maabara ya Shule ya Sekondari Msasani
iii) Ujenzi wa barabara – km. 2.5
iv) Ujenzi wa jingo la Utawala – Msasani Sekondari.


g) ELIMU YA MSINGI

Shule ya Msingi Kaloleni imeendelea kuboreka kitaaluma; mwaka jana wanafunzi 149 walifanya mtihani wa darasa la saba. Wavulana 70, wanawake 82; na kati yao waliofaulu ni 108. Wasichana 81 na wavulana 68.
Mwaka huu darasa la saba lina wanafunzi 168: wavulana 97 na wasichana 71. Changamoto kubwa hapa ni “Utoro sugu” kwani tuna wanafunzi wa kiume 15 ambao wanasumbua sana kwa utoro. Pia wazazi hawalipi ada za watoto wao kabisa.

h) ELIMU YA SEKONDARI

Shule ya sekondari Msasani imeendelea kukua na sasa tuna idadi ya madarasa 10 yanayotumiwa na manne yapo katika hatua ya msingi. Shule ina walimu 11, wanaume 4 na wanawake 7. Idadi ya wanafunzi ni 336: wanaume 174 na wasichana 162.

Ujenzi wa Shule:

Shule ya Msasani imejengwa na inaendelea kujengwa kwa ushirikiano wa wananchi, mradi wa TASAF, Manispaa ya Moshi na Wafadhili wengine kutoka nje ya nchi. Hadi January 2008 ujenzi huo unaweza kuchanganuliwa kama ifuatavyo:
Halmashauri: Millioni 51
Tasaf: Millioni 32
Wafadhili (Tasaf) Millioni 8
Wafadhili(ndani) Vifaa vya thamani: Millioni 9
Wafadhili (Ulaya) Vifaa vya thamani Millioni 9
Pia Kamati ya Maendeleo ya Kata imepokea msaada wa wafadhili kupitia International School of Moshi kama ifuatavyo:
-Cement mifuko 200 2,900,000 Tshs
-Matofali 3000 3, 600,000Tshs
-Mchanga lori 15 1,500,000 Tshs
*Jumla ya Thamani ya ufadhili wa vifaa ni Tshs. 9,040,000

MAHITAJI YA SHULE

Changamoto pekee kwa shule ni uchache wa walimu, ukosefu wa maabara, jiko, bwalo, Uzio wa shule (fence) na chumba cha kompyuta. Jitihada zinaendelea kutatua haya na mchango wa wananchi unategemewa sana hapa.

i)
SHULE ZA AWALI – CHEKECHEA

Watoto wadogo ndani ya Kata wanapata elimu yao kupitia shule kadha za chekechea: KKKT – Msasani, Al Hudda Nursery School, RC Chekechea, Kaloleni Nursery School.

j) TAASISI BINAFSI

Zipo taasisi binafsi mbili ambazo zinaendesha shughuli za huduma kwa wananchi wa Kaloleni na hata Kata za jirani:

a)
CCBRT
Ni taasisi ya huduma kwa watoto walemavu .

b) MUSLIM AGENCY

Ni taasisi ya Kiislamu ambayo inatoa huduma za kielimu kwa elimu ya awali, msingi, sekondari pamoja na huduma za afya.

k)
ULINZI NA USALAMA

Kata ya Kaloleni inapata huduma ya usalama kupitia kituo kidogo cha polisi. Kituo hiki kilijengwa kwa msaada kupitia Taasisi ya Muslim Agency. Kituo hiki kina askari mmoja polisi na askari mmoja mgambo.

l)
SHUGHULI NDOGONDOGO

Wakazi mbalimbali wa Kata ya Kaloleni wanajibidisha kufanya shughuli mbalimbali ili kujikimu. Kwa mfano: Mashine za kusaga, ufundi seremala, saluni za kiume na kike, Baa, maduka ya rejareja, utengenezaji masufuria, upikaji na uuzaji wa pombe za kienyeji ( Dadii na mbege).

m) ASASI ZA KIJAMII

Kata ya Kaloleni inazo asasi za kimazingira ambazo zinajihusisha kutunza vyanzo vya maji pamoja na kuhifadhi mazingira na moja inahusika na elimu ya uhamasishaji rika. Asasi hizi ni:

1. KEA GROUP
2. MVULENI GROUP
3. KALOLENI YOUTH GROUP